Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

Kongamano la Uwekezaji Songwe limekuja na mafanikio-Mashiba


Kongamano la Uwekezaji limemalizika Mkoani Songwe, Kongamano hilo lilikuwa na mafanikio makubwa kutokana na mwamko wa wawekezaji kushiriki katika Kongamano hilo lililokuwa na lengo la kuwaweka karibu wafanyabiashara na wawekezaji wa Mkoa huo pamoja na wafanyabiashara wa mikoa na mataifa mbalimbali Duniani.
Anaripoti Grace Semfuko aliehudhuria Kongamano hilo.

Kongamano hilo lililoandaliwa na Serikali ya Mkoa wa Songwe kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo limeleta chachu ya kuimarisha uwekezaji nchini hatua ambayo imefikiwa kufuatia juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli za kuimarisha sekta ya viwanda na uwekezani nchini.

Kituo cha Uwekezaji Tanzania TIC ni miongoni mwa Taasisi za Serikali zilizokuwa na nguvu katika kongamano hilo kutokana na ushiriki wake ikiwa ni sehemu ya kazi zake za kila siku za kuhakikisha uwekezaji Nchini Tanzania unakua kwa kiwango cha hali ya juu.

Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ya TIC ndio ilikuwa mwenyeji katika Kongamano hilo ambapo Meneja wake wa Kanda Bw. Venance Mashiba alisema Kanda hiyo inazo fursa nyingi za uwekezaji ikiwepo kwenye Kilimo, viwanda, Ujenzi na sekta nyingine nyingi ambapo hatua ya sasa ya TIC ni kuhakikisha wawekezaji wanapata elimu kuhusiana na kujiunga na Kituo hicho ili waweze kupata manufaa mengi ikiwepo vivutio vya kikodi.

“Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi sana, miongoni mwa rasilimali hizo ni pamoja na sekta ya kilimo, mfano kilimo cha Parachichi, Mahindi na mazao mengine, hii ni fursa yetu kubwa kwenye mikoa hii, nashauri wawekezaji wajiunge na kituo ili waweke kupata fursa nyingi” alisema Mashiba.

Kanda ya Nyanda za Juu Kusini inajumuisha Mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya na Rukwa ambapo kwa rasilimali, mikoa hii imebarikiwa kuwa na rasilimali za asili ikiwepo Madini mbalimbali, hali nzuri ya hewa kwa ajili ya kilimo, uvuvi pamoja na maeneo makubwa ya uwekezaji ambapo wawekezaji kutoka katika mataifa mbalimbali Duniani wanashauriwa kuwekeza kwenye mikoa hiyo.

Fursa nyingine za uwekezaji zilizopo kwenye mikoa hiyo ni pamoja na uwekezaji wa viwanda vya madawa na vifaa tiba pamoja na mafuta ya kipikia.

Aidha Mashiba aliyataja maeneo mengine ya uwekezaji kuwa ni kwenye uzalishaji wa zao la Kokoa ambapo Tanzania pekee inazalisha zaidi ya tani elf 10 za Kokoa huku maeneo ya Kyela yakiongoza.

“Kama mnavyofahamu Serikali ya awamu ya tano inasisitiza uwekezaji kwenye viwanda ili kuweza kusaidia maendeleo ya viwanda katika nchi yetu, na sisi TIC jukumu letu ni kuhakikisha tunatekeleza uhamasishaji na ufanikishaji wa ujenzi wa viwanda unaofanywa na wawekezaji wetu, tumejipanga kwa jambo hilo” alisema Mashiba.

Alisema kuwa eneo la kwanza ni kuahamasisha ujenzi wa viwanda vya kuchakata na kusindika mahindi. “ukiangalia maeneo ya Songwe, Mbeya, iringa na Rukwa ni mikoa ambayo inaongoza katika uzalishaji wa zao la mahindi”.

“TIC Nyanda za juu kusini inahamasisha uwekezaji wa viwanda vya kuchakata na kusindika mpunga, Wilaya ya Kyela pekee inazalisha tani elf 70 kwa mwaka huku Wilaya ya Mbarali ikizalisha tani laki 7, Songwe na Kamsamba yakizalisha mpunga kwa kiasi kikubwa sana, kwa hiyo uanzishwaji wa viwanda vya kuchakata mpunga vitasaidia ongezeko la uwekezaji katika mikoa ya Kanda hiyo”alisema Mashiba.


Post a Comment

0 Comments