Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

Taarifa za Uwekezaji ni kila baada ya miezi 6-Kairuki

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Uwekezaji Angellah Kairuki, amewataka wawekezaji waliosajili miradi yao kwenye Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), kuwasilisha taarifa za maendeleo na changamoto zao kila baada ya miezi sita ili ziweze kufanyiwa kazi za uboreshaji na utatuzi wa changamoto zake kwa wakati.

Anaandika Grace Semfuko, Dar es Salaam.

Kairuki alisema Kanuni za usajili za TIC zinawataka wawekezaji hao kufanya hivyo na kwamba hatua hiyo inalenga kuwaweka karibu wawekezaji hao ambao wamekuwa na tija ya kiuchumi kutokana na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali za viwandani na kilimo ambazo hutoa ajira kwa watanzania na ulipaji kodi unaostahili.

Aliyasema hayo alipotembelea kiwanda cha OK Plastic Limited kilichopo Vingunguti Jijini Dar Es Salaam kinachochakata bidhaa(vyuma) chakavu na kuzalisha rodi za shaba, nyaya za umeme, betri ingots na mikeka ambacho kimeajiri wafanyakazi 595 wa kitanzania na raia wa kigeni watano.

“Nawasihi wawekezaji wote mliojisajili na TIC, pelekeni taarifa zenu za maendeleo ya miradi yenu kila baada ya miezi sita ili tujue ni wapi kuna changamoto tuweze kuzitatua kwa wakati, ni kwa nia njema sana, Serikali yenu ipo na ni sikivu, pia naomba niwapongeza wamiliki wa kiwanda hiki cha OK kwa ulipaji wa kodi mzuri na mmeajiri watanzania wengi, na wengine igeni mfano wa kiwanda hiki” alisema Waziri Kairuki.

Meneja wa kiwanda hicho Bw.Fadil Ghaddar alisema uwekezaji wao kwa sasa umefikia shilingi Bil 10 na kwamba tangu kuanzishwa kwake mwaka 2005 wamepata mafanikio makubwa ikiwepo soko la uhakika la ndani ya nchi pamoja na baadhi ya nchi jirani ikiwepo Kenya.
Mbali na uzalishaji wa bidhaa hizo, kiwanda hicho pia kinatoa mafunzo ya utengenezaji wa bidhaa mbalimbali za metali kwa vijana waajiriwa wao ili kuwajenga kiuchumi kwa kuanzisha viwanda vyao pindi wanapoamua kuacha kufanya kazi kiwandani hapo.

Kiwanda hicho kinalipa kodi ya mapato ya zaidi ya shilingi Bilioni 2 kwa mwaka, lakini wanasema changamoto yao kubwa ni upatikanaji wa malighafi za uzalishaji wa bidhaa na wameiomba Serikali iweke mikakati ya kuhakikisha kwamba viwanda vya ndani vinapata malighafi kwanza ya kutosheleza au kuweka zuio kabla ya uuzwaji wa malighafi hizo nje ya nchi ambapo Waziri Kairuki  alisema amelipokea ombi hilo na ataliwasilisha kwenye mamlaka zinazohusika ili ziweze kulifanyia kazi.

“Mheshimiwa Waziri, hapa kiwandani tunayo changamoto ya upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa hizi, hali hii imetufanya kupunguza uzalishaji kutoka tani 500 za shaba kwa mwezi hadi kufikia tani 150 tu, utafiti uliofanywa na Taasisi ya BICO ya chuo kikuu cha Dar es Salaam hivi karibuni ulionyesha kuna upatikanaji wa kutosha wa bidhaa chakavu za shaba nchini kiasi cha kutosheleza viwanda vya ndani, lakini tunakwama kupata malighafi hiyo kwa sababu inauzwa nje, tunaiomba Serikali izuie ili tupate sisi” alisema Ghaddar.

Alisema wanatumia fedha nyingi kuagiza malighafi za shaba kutoka nje ya nchi na kwamba iwapo Serikali itazuia bidhaa hizo kuuzwa nje ya nchi itakuwa ni nafuu kwao.
Mwisho.

Post a Comment

0 Comments