Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

Tanchoice Pwani kunufaisha uwekezaji wa mifugo.

Sekta ya mifugo ni miongoni mwa sekta za kipaumbele katika uwekezaji, Serikali ya Tanzania imekuwa ikihimiza uwekezaji kwenye sekta hii ambayo imekuwa na tija ya kiuchumi.




Hivi ndivyo kiwanda cha Tanchoice kitakavyohifadhi nyama kwa ajili ya kuuzwa ndani na nchi  huku nyingine itasafirishwa kwa ajili ya mauzo katika nchi za nje.

Anaandika Grace Semfuko
Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikiweka mikakati ya kuhakikisha afya ya mifugo zinaimarishwa vyema pamoja na kuwezesha upatikanaji endelevu wa rasilimali za vyakula na maji kwa ajili ya mifugo.
Mikakati mingine ni kuboresha biashara ya mifugo ndani na nje, kuimarisha huduma za utafiti wa mifugo, huduma za ugani na mafunzo kwa wafugaji na maafisa ugani, kuanzisha na kuimarisha vikundi na vyama vya ushirika vya mazao ya mifugo, kuboresha utekelezaji wa sera, sheria na kanuni katika sekta ya mifugo pamoja na kuimarisha uratibu na usimamizi wa wataalamu wa sekta ya mifugo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Uwekezaji Angellah Kairuki akiwa katika picha ya pamoja na Wafanyakazi wa Kiwanda cha nyama cha Tanchoice alipotembelea kiwanda  hicho hivi karibuni.



Katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuboresha nyororo wa thamani kwenye sekta ya nyama Kampuni ya Tanchoice Limited imejenga kiwanda kikubwa katika Wilaya ya Kibaha Mkoa wa Pwani kitakachokuwa na uwezo wa kuchinja mifugo zaidi ya elf 5 kwa siku na kuzalisha nyama ambayo itauzwa ndani na nje ya nchi.
Kiwanda hicho kimejengwa kwa gharama ya shilingi Bilioni 23 kinakadiriwa kutoa ajira ya zaidi ya watu 500.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Uwekezaji Angellah Kairuki akitoa neno katika Kiwanda cha nyama cha Tanchoice hivi karibuni baada ya kutembelea hicho.


Kiwanda hicho ambacho kitakuwa na migawanyo mitano ya machinjio kitakuwa ni kiwanda kikubwa cha nyama kwa nchi za Afrika Mashariki na cha pili kwa ukubwa Barani Afrika kikitanguliwa na kile cha nchini Ethiopia ambacho kina uwezo wa kuchinja ng’ombe 3,000, mbuzi na kondoo 6,000 na kuzalisha tani 3,000 za nyama kwa siku moja. 

Akizungumza mara baada ya kukagua ujenzi wa kiwanda hicho, Kaimu Msajili wa Bodi ya nyama Tanzania Iman Sichalwe alisema kiwanda hicho ni kikubwa kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati kwenye Sekta ya mifugo na kwamba kukamilika kwake kutaleta tija kwa wafugaji na kuinua sekta ya mifugo nchini.

Sichalwe alisema kwa sasa kiwanda hicho kimefikia asilimia zaidi ya 90 na kwamba muda wowote kitaanza kufanya kazi kwa hiyo ni nafasi nzuri kwa wafugaji kuchangamkia fursa hiyo kwa kufanya ufugaji wa kisasa ambao mifugo yake itakidhi mahitaji ya kiwanda hicho.

“Sehemu ya kufikia wanyama tayari, sehemu ya kuchinjia tayari mashine zote zimeshafungwa, maabara na vitu vyote vimekamilika ikiwepo cheti cha kibali cha bodi ya nyama” alisema Sichalwe.
Meneja uzalishaji wa Kiwanda hicho Selo Luhongo alisema asilimia 20 ya nyama itakayochinjwa kiwandani hapo itauzwa ndani ya nchi huku asilimia 80 zilizobakia zitauzwa nje ya nchi.

“Tumeshafikia asilimia 99.9 ya ukamilishaji wa ujenzi wa kiwanda hiki ili kianze rasmi kazi iliyokusudiwa, tunawaomba wafugaji na wadau wote wa sekta hii wakiwepo wafugaji, wasafirishaji na wafanyabiashara wazingatie kanuni za afya na ustawi wa wanyama” alisema Luhongo.

Juhudi za Serikali za kuimarisha sekta ya mifugo na mazao ya nyama zinafanyika ambapo katika hotuba ya makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya 2020/2021 Bungeni Jijini Dodoma, Waziri wa Wizara hiyo Luhaga Joelson Mpina alisema idadi ya mifugo nchini inakadiriwa kuongezeka ikilinganishwa na mwaka 2018/2019 ambapo idadi ya ng’ombe imeongezeka kutoka milioni 32.23 hadi milioni 33.4, mbuzi kutoka milioni 20 hadi milioni 21.29 na kondoo kutoka milioni 5.5 hadi milioni 5.65.

Kuongezeka kwa idadi hiyo kunatokana na sera na mifumo thabiti ya utunzaji na ulinzi wa mifugo na kusababisha kuongezeka kwa uzalishaji wa zao la nyama kutoka tani 690,629 mwaka 2018/2019 hadi tani 701,679.1 mwaka 2019/2020 sawa na ongezeko la asilimia 1.6 kati ya hizo, tani 486,736.1 za nyama ya ng’ombe, tani 95,964.2 za nyama ya mbuzi na kondoo, tani 80,601.3 za nyama ya kuku na tani 38,377.4 za nyama ya nguruwe. 

Aidha, ng’ombe walionenepeshwa wameongezeka kutoka ng’ombe 371,200 mwaka 2018/2019 hadi kufikia ng’ombe 512,256 mwaka 2019/2020 sawa na ongezeko la asilimia 38.

Aidha katika mazao ya ngozi Waziri Mpina alisema hadi kufikia Aprili 30, 2020 jumla ya kilo za ngozi 16,746,589.36 kutoka kwenye ng’ombe 14,449,075.49, mbuzi 1,775,298.5 na kondoo 522,215.38 zenye thamani ya shilingi bilioni 23.9 zimezalishwa ikilinganishwa na kilo 16,012,800.71 za kutoka kwenye ng’ombe 13,904,620.27, mbuzi 1,653,669.26 na kondoo 454,511.17 zenye thamani ya shilingi bilioni 22.8 zilizozalishwa mwaka 2018/2019.

Alisema hadi kufikia Machi 30 mwaka huu Sekali imeingiza zaidi ya shilingi Bilioni 12.9 za mauzo ya ngozi za wanyama hao kwenye nchi za Ghana, China, Pakistani, Indonesia, Ethiopia, Nigeria na Italy ikilinganishwa na mauzo ya shilingi bilioni 13.0 ya mwaka mwaka 2018/2019.

Katika mwaka 2019/2020, Wizara kupitia Fungu 99 ilitarajia kukusanya kiasi cha shilingi Bilioni 50 ambapo hadi kufikia Aprili 30, 2020 zilikusanywa shilingi Bil. 38.5 sawa na asilimia 77 ya lengo la makusanyo ya mwaka huo wa fedha.

Aidha Wizara hiyo imeendelea kupitia Sheria za sekta ya mifugo kwa ajili ya kuboresha mazingira na kuwezesha ukuaji wa sekta ya mifugo ambapo marekebisho ya Sheria za Ustawi wa Wanyama na Sheria ya Magonjwa ya Mifugo yamefanyika kupitia Written Laws Miscelleneous Amendments Act 2019, Act No.14 of 2019

Mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Nyanda za Malisho na Rasilimali za Vyakula vya Mifugo SURA 180 yaliyopo katika Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Written Laws Miscelleneous Amendments Act 2020) tayari yameshasomwa kwa mara ya kwanza katika kikao cha Bunge la Mwezi Januari, 2020.

Wizara imeandaa Kanuni mbalimbali chini ya Sheria ya Magonjwa ya Wanyama na kutangaza katika Gazeti la Serikali kwa ajili ya kuanza kutumika ili kutatua changamoto mbalimbali katika Sekta ya Mifugo.

Wizara imefanya marekebisho ya tozo katika Kanuni za Magonjwa ya Wanyama na kuwasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango. Aidha, kanuni mbalimbali chini ya Sheria ya Veterinari zimeandaliwa na kutangazwa katika Gazeti la Serikali kwa ajili ya kuanza kutumika.


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments