Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

TIC yapanda mbegu kwa Vijana nchini; Kuanzisha uwekezaji binafsi ili kutatua changamoto ya ajira



Mkurugenzi Mtendaji akijibu maswali ya washiriki baada ya kuwasilisha hotuba yake

Suala la ukuzaji wa kada ya ujasiriamali mdogo na wa kati (SME) siyo tu limesisitizwa na Ilani ya Chama Tawala, bali pia ni utekelezaji wa majukumu ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kama lilivyoanishwa na Mpango Mkakati wa Kituo 2016-2021. Ni katika kutekeleza majukumu hayo Geoffrey Mwambe, Mkurugenzi Mtendaji wa TIC ameshiriki kama Mgeni Rasmi katika Kongamano la Uchumi na Uwekezaji lililoandaliwa na UVCCM SENETI Mtwara kwenye ukumbi wa Stella Maris University Mtwara tarehe 30 Machi, 2019. Lengo la kongamano lilikuwa ni kujadili uwekezaji unavyotatua changamaoto za ajira kwa vijana.
Sehemu ya washiriki wa kongamano


Hotuba ya mgeni rasmi, ilijawa na maneno ya hamasa kwa vijana ambapo amewataka kujiamini na kuthubutu katika kuibua na kutekeleza miradi ya uchumi kwenye sekta za kipaumbele ambazo ni kilimo, viwanda, madini, mifugo na uvuvi. Washiriki wameelezwa kutafiti na kutambua fursa zinazowazunguka mahali walipo na kuibua miradi ya uwekezaji inayoweza kutekelezwa kwa lengo la kutengeneza ajira na kuzalisha bidhaa au huduma zinazolenga kuinufaisha jamii na Taifa kwa ujumla. Kwa muktadha huo vijana wameelezwa kwamba mtazamo wao wa kwanza wa kupata ajira iwe ni ile inayotokana na uwekezaji wao wenyewe/ kujiajiri. Hivyo kujiamini na kuthubutu ni hatua kwa vijana katika kutengeneza ajira badala ya kutegemea dhana iliyozoeleka ya kutafuta ama kusubiri kuajiriwa. 

Washiriki waliposimamam kumkaribisha Mgeni Rasmi Geoffrey Mwambe alipokuwa akiingia ukumbini


Elimu ya uwekezaji na uchumi iliyotolewa kupitia kongamno hilo, inatafsiriwa kuwa ni mbegu bora ya maendeleo iliyopandwa kwa takribani washiriki 600 wengi wao wakiwa vijana ambao ni wawekezaji watarajiwa kwa jamii ya Watanzania na Taifa kiujumla. Kinachotakiwa ni vijana kuanza utekelezaji wa kuyaishi yote waliyoelekezwa ikiwa ni pamoja na kuanzisha vikundi vya watu watano sambamba na kusajili kampuni. Baada ya kusajili kampuni wafuate hatua inayofuata ya kubuni/kuibua miradi mbalimbali ya uchumi kwa utekelezaji. Mwambe alisema ‘utekelezaji wa uanzishaji wa vikundi ni hatua muhimu kwa vijana kutokana na ukweli kwamba itawasaidia kunufaika na vyanzo vya fedha za uwezeshaji kutoka Serikalini na sekta binafsi inayotolewa kupitia kwenye vikundi kwa ajili ya mitaji ya kutekeleza shughuli/miradi ya kiuchumi na uwekezaji .


Mmoja wa Walimu wa Chuo cha Stella Maris University akichangia hoja juu ya Serikali kusisisitiza utekelezaji wa sera ya kujitegemea kwa wanavyuo kam ilivyokuwa zamani

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu. Mhe Moses Machali alitumia kongamano hilo pia kutoa ufafanuzi zaidi ya kwamba vijana waamke kutumia fursa za uwekezaji zilizopo ili kuibua miradi ya uchumi na uwekezaji katika maeneo yanayowazunguka. Vijana kuweni na tabia ya kujishughulisha kutekeleza miradi ya kiuchumi ikilenga maeneo ya uzalishaji, usambazaji na ulaji. Kwa msisitizo Mhe.Machali alisema ‘Vijana wakati huu ni wa kupambana na kuthubutu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. Ni wajibu wa vijana kuchukua hatua kwa vitendo katika kuanzisha miradi ambayo itachangia kwenye maeneo matatu makuu ya uchumi ambayo ni uzalishaji ‘production’ usambazaji ‘distribution’ na ulaji ‘consumption’. 


Mwanafunzi wa mwaka wa pili akieleza namna ambavyo wanafunzi wanatakiwa kuzingatia elimu wanayopewa ili wanapohitimu waweze kuitumia kivitendo katika sehemu zao za kazi.


Mwambe amewahakikishia wadau wengine utayari wa Kituo kushiriki kwenye makongamano ya aina hiyo yenye lengo la kutoa elimu kwa washiriki juu ya uchumi na uwekezaji kwa manufaa ya nchi yetu. Mwisho, anawakaribisha wadau wote kutembelea ofisi za TIC zinazopatikana Dar es Salaam Makao Makuu mtaa wa Shabaan Robert na katika Ofisi za TIC za Kanda zinazopatikana nchini. Lengo ni kupata miongozo na kushauriana/kujadiliana namna ya kuibua na kuanzisha miradi ya uwekezaji kupitia fursa zinazopatikana katika maeneo yanayotuzunguka. Akitambulisha Ofisi za Kanda Mwambe amesema, Ofisi za TIC Kanda ya Kusini zinapatikana Mtwara Jengo la Mkuu wa Mkoa, Ofisi za TIC Kanda ya Mashariki zinapatikana Dar es Salama Jengo la TIC Makao Makuu, Ofisi za TIC Kanda ya Kati zinapatikana Dodoma Jengo la Manispaa, Ofisi za TIC Kanda ya Magharibi zinapatikana Kigoma Jengo la Mkuu wa Mkoa, ofisi za TIC Kanda ya Kaskazini zinapatikana Moshi Jengo la Mkuu wa Mkoa, Ofisi za TIC Kanda ya Ziwa zinapatikana Mwanza Barabara ya Kenyatta na ofisi za TIC Kanda ya Nyanda ya Juu Kusini zinapatikana Mbeya Jengo la Benki ya NBC.

Post a Comment

0 Comments