Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

Serikali Kuiongezea Mtaji TADB isaidie Wawekezaji Wadogo-Kairuki

Serikali imeahidi kuiongezea mtaji Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ili kuendelea kuwasaidia Wakulima katika uwekezaji wa sekta hiyo.

 Anaandika Grace Semfuko

TADB inaendelea kuwasaidia Wakulima na kuwapa kipaumbele wawekezaji wazawa.

Hayo yalisemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Uwekezaji Angellah Kairuki mwishoni mwa wiki alipofanya ziara katika kiwanda cha kuchakata mbegu za Alizeti cha Qstek Wilayani Manyoni Mkoa wa Singida ambapo aliipongeza Benki hiyo kwa kueleza kuwa imekuwa ikiwainua Wakulima na wawekezaji wadogo tofauti na taasisi zingine za fedha.

Aliipongeza Benki hiyo kwa kutoa mkopo wa shilingi Bilioni 2.2 kwa wawekezaji hao wa Qstek kwa ajili ya uwekezaji wao,kiwanda kitakachokuwa na uwezo wa kuchakata mbegu za alizeti tani 6,000 kwa mwaka na kuzalisha mafuta ya kula yenye ubora tani 2,500 kwa mwaka.

 “Niwapongeze sana TADB kwa namna mnavyowashika mkono Wakulima, mtaji wa shilingi Bilioni 2.2 mlioutoa hapa ni mkubwa, niwasihi muendelee kuwawezesha zaidi hadi watakaposimama kabisa, nafahamu pia mmewezesha wakulima 829 na mnao mpango wa kuwawezesha wengine laki mbili” alisema Kairuki.

“Onesheni mfano wa kuwasaidia Wakulima na Vijana wetu ili kwa pamoja tuweze kufikia malengo na ndoto za Rais wetu Dkt John Pombe Magufuli kwamba ifikapo 2025 tufikie uchumi wa kati unaotegemea viwanda” alisisitiza Waziri Kairuki.


Aliongeza kuwa Serikali imeweka unafuu wa kikodi kwa wawekezaji ili kuvutia uwekezaji na kuwataka Wakurugenzi wa Halmashauri Nchini kutenga maeneo ya uwekezaji na kutowakwamisha wawekezaji wanaotaka kuwekeza viwanda na miradi mbalimbali.


Mkurugenzi wa Benki ya TADB Japhet Justine alisema mpaka sasa ujenzi wa mradi huo umegharimu shilingi Bilioni 3huku wao kama wadau wa maendeleo wametoa shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya kusaidia gharama za ujenzi  wa majengo ya kiwanda na shilingi milioni 718 kwa ajili ya kusaidia kuanzisha uzalishaji.


Alisema Tanzania kwa viwanda vya mafuta vilivyopo inazalisha tani 201,000 bado havitoshi na kuongeza kuwa njia pekee ya kufanya mapinduzi katika katika sekta ya mafuta ni kuwezesha wakulima wadogowadogo kufanya kilimo cha kisasa.


“Tunapaswa kuwasaidia Wakulima wadogo wadogo na sisi kama benki ya maendeleo ya kilimo tumeshaanza kuchukua hatua ya kuhakikisha wakulima hawa wanahama kutoka kwenye ule mfumo wa kutumia mbegu ambazo walizitumia mwaka jana na msimu mpya ukianza wanazitumia tena, tayaru tumeshaanza kulifanyia kazi suala hilo” alisema.


Aliongeza kuwa “tunaamini tukihamasisha kuwainua wakulima wadogowadogo, tutawainua wengi hapa Manyoni na sehemu nyingine nchini, kwa hiyo nikuahidi tutaendelea kushirikiana na Mkoa wa Singida kuwainua wakulima wa alizeti ambao tunaamini wakiinuka wao na Singida imenyanyuka” aliongeza.


Alisema huo ni mkopo wao wa pili kuutoa ndani ya mkoa huo ambapo tayari wametoa zaidi ya shilingi milioni 600 kwa wakulima wadogowadogo waliokuwa wanazalisha alizeti pamoja nan a hizo shilingi Bilioni 2.2 kwa ajili ya kiwanda hicho cha Qstek lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi inayoongoza kuuza mafuta ya alizeti nje ya nchi.


Mkurugenzi wa kiwanda hicho Emmanuel Nagunwa aliishukuru Serikali kwa kuwawezesha kuanzisha kiwanda hichoambacho kitaongeza wigo wa biashara ya zao la alizeti na kuchochea mapato kupitia kodi mbalimbali zinazotokana na uzalishaji wa kiwanda hicho.

Post a Comment

0 Comments