Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

Wawekezaji wa Ok Plast waiangukia Serikali kuhusu malighafi


Na Mwandishi wetu, Dar Es Salaam.
Wawekezaji wa Kiwanda cha OK Plastic Limited cha Vingunguti Jijini Dar Es Salaam ameiomba Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) kusitisha uuzwaji wa malighafi za shaba nje ya nchi zoezi linalofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wa ndani kwa kuwa linawapunguzia upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa viwanda vya ndani na hivyo kupunguza uzalishaji kwenye viwanda vyao.

Kiwanda cha Ok Plastic Limited kilichokuwa na uwezo wa kuzalisha bidhaa za shaba tano 500 kwa mwezi, hivi sasa kinazalisha tani 150 tu kutokana na kukosekana kwa malighafi hiyo ndani ya nchi hatua ambayo amesema inawapa changamoto kubwa kiwandani hapo.

Hayo yalibainishwa na Meneja wa Kiwanda hicho Bw. Fadil Ghaddar kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anaeshughulikia Uwekezaji Angellah Kairuki aliyetembelea kiwandani hapo ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ambapo alisema iwapo Serikali itazuia uuzwaji holela wa bidhaa hiyo nje ya nchi, itaongeza uzalishaji wa viwanda vya ndani.

“Mheshimiwa Waziri, sisi changamoto yetu kubwa ni malighafi ya shaba kiwandani kwetu, malighafi hii ipo nyingi nay a kutosha hapa nchini kwani kuna utafiti ulifanywa na Taasisi ya  BICO ya chuo kikuu cha Dar es Salaam ambao ulionyesha kuna upatikanaji wa kutosha wa bidhaa hiyo, tunakuomba utuwasilishie ombi letu la kusitisha uuzwaji nje ya nchi wa malighafi hizo, kwani nasi tunapoagiza hujo nje tunatumia gharama kubwa sana” alisema Bw. Ghaddar.

Kwa upande wake Waziri Kairuki alisema amepokea ombi lao hilo na ataliwasilisha kwenye mamlaka zinazohusika.

“Nimelipokea ombi lenu na nitaliwasilisha kwenye mamlaka zinazohusika, nipende tu kuwahakikishia Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji kila mara na nyie ni mashahidi kwani tumeboresha Sera na sheria zetu ili kuwarahisishia uwekezaji wenye tija” alisema Waziri Kairuki.

Aidha katika hatua nyingine Waziri Kairuki, amewataka wawekezaji waliosajili miradi yao kwenye Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), kuwasilisha taarifa za maendeleo na changamoto zao kila baada ya miezi sita ili ziweze kufanyiwa kazi za uboreshaji na utatuzi wa changamoto zake.

Kairuki alisema Kanuni za usajili za TIC zinawataka wawekezaji hao kufanya hivyo na kwamba hatua hiyo inalenga kuwaweka karibu wawekezaji hao ambao wamekuwa na tija ya kiuchumi kutokana na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali za viwandani na kilimo ambazo hutoa ajira kwa watanzania na ulipaji kodi unaostahili. 

“Nawasihi wawekezaji wote mliojisajili na TIC, pelekeni taarifa zenu za maendeleo ya miradi yenu kila baada ya miezi sita ili tujue ni wapi kuna changamoto tuweze kuzitatua, ni kwa nia njema sana, Serikali yenu ipo na ni sikivu, pia naomba nawapongeza wamiliki wa kiwanda hiki cha OK kwa ulipaji wa kodi mzuri na mmeajiri watanzania wengi, na wengine igeni mfano wa kiwanda hiki” alisema Waziri Kairuki.

Kiwanda cha OK Plast Limited tangu kuanzishwa kwake mwaka 2005 kimekuwa na mafanikio makubwa ya soko la bidhaa zake nchini Tanzania nan chi jirani ikiwepo Kenya, Kiwanda hiki kimewekeza nchini kwa mtaji wa Shilingi Bilioni 10 na kinazalisha bidhaa za nyaya za umeme,betri ingots na mikeka, kimeajiri wafanyakazi 595 wa kitanzania na raia wa kigeni watano.

Mwisho.


Post a Comment

0 Comments