Header Ads Widget

Ticker

6/recent/ticker-posts

Miaka Mitano ya Magufuli tumesajili Uwekezaji Mkubwa TIC-Mwambe


Kituo cha Uwekezaji Tanzania -TIC katika kipindi cha Januari 2016 hadi Juni 2020 kimefanikiwa kusajili jumla ya miradi 1,312 ya uwekezaji yenye mtaji wa thamani ya Dola za Kimarekani Bilioni 20 ikiwa ni takribani Shilingi Trilioni 46 za kitanzania na kutoa ajira ya Watanzania 178,101.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania Bw. Geoffrey Mwambe akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam kuhusu mafanikio ya TIC katika kipindi cha Miaka mitano ya Uongozi wa Rais Dkt John Pombe Magufuli.

Anaandika Grace Semfuko kutoka Dar es Salaam.

Katika usajili huo sekta ya uzalishaji na usindikaji wa viwanda iliongoza kwa asilimia 54 ya miradi yote na ilitoa ajira kwa watanzania 67,992.

Akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam kuhusu mafanikio ya miaka mitano ya TIC, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo hicho Bw. Geoffrey Mwambe, amesema tangu kuingia madarakani kwa Rais Dkt John Pombe Magufuli, kumekuwa na mafanikio makubwa ya kujivunia kwenye Sekta ya Uwekezaji.

“Katika Serikali ya awamu ya tano, Kituo kimeendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano, dira yetu ilikuwa ni kuwa Kituo bora kabisa Duniani kwa kuvutia uwekezaji wa maendeleo endelevu”alisema Mwambe.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania Bw. Geoffrey Mwambe akisisitiza jambo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam kuhusu mafanikio ya TIC katika kipindi cha Miaka mitano ya Uongozi wa Rais Dkt John Pombe Magufuli.

Amesema Tanzania inao uwezo mkubwa wa kufanya maendeleo ya kasi kwamba ndani ya miaka mitano tu hali ya uchumi na maendeleo ya Taifa yamebalidika kwa kiwango kikubwa kuliko ilivyotarajiwa.

“Watanzania tunapaswa kujivunia, ndani ya miaka mitano tumebadili kabisa hali yetu ya uchumi na maendeleo ya Taifa, watu wanaokuja hawaamini kwamba hii ni Tanzania ile waliyokuwa wanaijua awali, ambayo hatukuwa na uwezo wa kutengeneza miundombinu yetu kama Reli ya kisasa ya SGR, wanabakia tu kuhoji Tanzania mnaweza? Sisi tunasema ndio tunaweza” alisisitiza Mwambe.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania Bw. Geoffrey Mwambe akizungumza na Waandishi wa Habari Jijini Dar Es Salaam kuhusu mafanikio ya TIC katika kipindi cha Miaka mitano ya Uongozi wa Rais Dkt John Pombe Magufuli.

Alizungumzia pia uboreshaji wa TIC kwenye huduma za mahala pamoja (One Stop Facilitation Centre) akisema, zimeboreshwa kwa kuongeza idadi ya taasisi zinazohudumia Wawekezaji kutoka taasisi saba mwaka 2015 hadi kufikia 10 mwaka 2020, huku idadi ya watumishi katika eneo hilo wakiongezeka kutoka 14 wa awali, na kufikia 25 lengo likiwa ni kumrahisishia Mwekezaji. 

Kuhusu kusogeza huduma za Uwekezaji kwenye maeneo yote nchini Mwambe amesema ofisi za Kanda za TIC zimeongezeka kutoka kanda tatu zilizokuwepo awali mwaka 2015 na kufikia Kanda Saba kwa mwaka 2020zikiwepo za Kanda ya Ziwa, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Kanda ya Kaskazini, Kati, Magharibi na Mashariki.

Aidha alizungumzia pia hatua ya TIC ya kuanzisha kamati ya Taifa ya uwezeshaji Uwekezaji (NIFC) ambayo inahusisha Wakuu wa Taasisi za Serikali zinazotoa vibali na leseni mbalimbali za uwekezaji yenye jukumu la kusaidia kuondokana na changamoto za sekta hiyo kwenye maeneo yanayosimamiwa na Taasisi hizo.

Katika hatua nyingine Mwambe amesema TIC imeboresha mifumo ya kuchakata na kutoa vibali kwa njia ya mtandao ikiwpo utoaji wa cheti cha vivutio, usajili wa Kampuni pamoja na Vibali vya kazi na ukaazi lengo likiwa ni kuwa na mkakati wa pamoja wa kushirikiana katika shughuli zote za uhamasishaji, Uwekezaji na Biashara.

 Kwa upande wa tafiti zinazofanywa na kituo hicho Mwambe amesema umefanyika utafiti kuhusu mwenendo wa mitaji ya uwekezaji kutoka nje ili kubaini hali halisi ya ukuaji, fursa na changamoto za kisekta ili kuziboresha huku akizitaja tafiti hizo kuhusika kwenye maeneo ya kilimo, mifugo, viwanda na mazingira ya biashara kwa ujumla. 

Katika mkutano huo na Waandishi wa Habari Mwambe pia alitoa matokeo ya tafiti za athari za uwekezaji zilizofanywa kufuatia kuibuka kwa ugonjwa wa Homa kali ya mapafu (COVID-19) kwa wawekezaji wa miradi iliyosajiliwa na TIC huku akiitaja sekta ya utalii na viwanda vya uchakataji vinavyotegemea malighafi toka nje ya nchi.

Alisema katika kipindi cha COVID-19 TIC iliendelea kufanya kazi kwa ustadi mkubwa na kuboresha mifumo ya utendaji kazi kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu wa Afya
Mwisho.

Post a Comment

0 Comments